Friday, July 22, 2016

Msukumo / motisha

Endelea kukimbia hata kama ni wa mwisho katika mashindano. Huwezi jua, yawezekama ukawa bingwa.

Ninawakummbusha ndugu zanguni kutokata tamaa maana muda unaokata tamaa unaweza kuwa ndio muda sahihi kabisa kwa wewe kupata mafanikio/ ukitakacho/ ulichoomba kwa muda mrefu/ kufikia ndoto zako na kadhalika.

Ukihisi kuacha usiache, kazana kwa kuwa umekaribia. Sote ni washindi kwa muda tofauti na kwa namna tofauti.

Thursday, July 21, 2016

Kila lililokamilika huanza kwa uamuzi wa kujaribu.


Msemo wa leo ni wa kutuhamasisha zaidi. Kila lililokamilika huanza kwa uamuzi wa kujaribu.

Chukua mfano huu mdogo. Umekaa kochini ukatamani maji ya kunywa lakini unaona uvivu kunyanyuka, hutapata maji. Kuna watu ndani unashindwa kuwaomba msaada wakuletee, hutapata maji. Umepata ila ni ya moto unahitaji ya baridi na huchukui uamuzi wowote, hutakata kiu yako.

Sasa, unataka kufanikisha mipango yako ambayo pengine hujaanza hata kujipanga, hutaikamilisha. Inatakiwa ifikie wakati ambapo utasimama hata kama umechoka au hujiwezi kufedha au kimwili. Anza safari huku ukiomuomba Mungu, naye atakuimarisha ukiwa njiani na utafika salama.

Fanya maamuzi haraka ya wapi uanze ama wapi upite na sio maamuzi ya kuendelea kusubiri. Bora ujaribu ushindwe kuliko usijaribu kumbe unajikosesha faida. Na ukijaribu ukashindwa usikate tamaa haraka, jaribu tena na tena mpaka utakapoona haiwezekani kabisa; ingawaje hakuna lisilowezekana kwa Mungu. Utachelewa lakini sio kushindwa.

Kazi kwako...

Wednesday, July 20, 2016

Onyesha heshima hata kwa watu wasiostahili; sio kwa muonekano wa tabia zao ila muonekano wa yako.


Maneno ya Dave Willis yanakumbushia utoaji wa heshima. Waswahili wanasema "heshima ni kitu cha bure" yaani huhitaji kulipia wala kugharamia chochote kuheshimu ama kuheshimiwa ila kujiheshimu na kutoa heshima hiyo kwa wengine wote hata kama hawastahili heshima yako.

Inakuwaje mtu hastahili heshima yako? Ni kwa sababu haonyeshi upendo kwako kama binadamu, sababu anakuona uko chini sana, sababu anakudharau, anakuona hufai kwake na katika maisha yake, sababu huna uwezo kifedha ama kifikra, sababu huwezi kufika alipofika, sababu hujampa alichotaka, hauna muonekano mzuri na mengine mengi.

Zipo sababu nyingi lakini pamoja na yote tunapaswa kukumbuka kuwa sote ni binadamu na tunakosea. Inawezekana tukapishana leo  lakini tukumbuke dunia huzunguka, binadamu pia. Tuheshimiane kwani hatujui ya kesho, inawezekana ukamheshimu mtu leo hata kama hastahili na kesho akawa msaada mkubwa tu kwako. Lakini tukijikweza leo, kesho tutaaibika.

Usimuhemu huyu ukamuacha yule ukidhani unakuwa mwema zaidi. Heshimu wote ili uonekane mwenye heshima.

AFRITRACUL




 Hivi ni vitu vya kiafrika kabisa. Vaa upendeze. Pendeza nasi AFRITRACUL kwa bei nzuri kabisa. Unaweza kutoa oda ya kitu ukitakacho ukatengenezewa. Jumla na reja reja unapata. Karibuni nyote.
























Tuesday, July 12, 2016

AFYA ni nini?


Afya ni hali ya kutokuwa na ugonjwa au kidonda. Afya ni hali ya kuwa na amani ya roho. Afya ni ubora wa akili, mwili na nafsi. Afya hutegemea vitu hivi vitatu kuwa ili kuwa hai na salama:
  • Akili
  • Mwili
  • Nafsi
Akili ni utashi tuliopewa na Mwenyezi Mungu katika kung'amua mambo ulimwenguni. Akili hujumuisha uelewa, ufikiri, uamuzi na utendaji wa mambo. Hakuna awezaye kutafsiri akili yetu ila matendo yetu yanaweza kumfanya mtu aone flani yuko vipi; nayo bado itakuwa mtazamo wake sababu tunatofautiana kufikiri pia. 

Binadamu hutumia akili kila siku na kila wakati ili kuelewa, kufikiri, kuamua na kuhakikisha tunatimiza jambo. Kwa maana hiyo, tunapaswa kuipumzisha "PUMZISHA AKILI". Akili ikichoka mwili nao huchoka na hutafanya chochote sababu haitakuwa na uwezo mzuri kutenda. Lala au oga au ogelea au sikiliza mziki au chochote ukipendacho ambacho hakitakufanya utumie nguvu ya akili.

Mwili ni muundo wote wa binaadam. Ni maumbile ya mtu. Mwili huhusisha yote yaliyotengeneza "mtu" mfano viungo kama miguu, mikono n.k, Maji kama mate, damu n.k, na vingine kama mishipa kucha na nywele.

Tunapaswa kujipenda kwa kula vizuri, kulala vizuri na pazuri, kuvaa vizuri na kujijali muda wote kwa kuuweka mwili salama mfano kwa kupiga mswaki baada ya kula, kuosha nywele mara kwa mara, kukata na kusafisha kucha, kuoga, na kuvaa nguo safi. Pia tujiepushe na hatari, ugomvi na makwazo kwa faida ya mioyo yetu. 

Ukitembea sana juani pata kivuli unywe na maji. Penye baridi uvike mwili wako kwa sweta ama nguo nzito. Ukiumia au kuumwa pata matibabu sahihi kwa kwenda hospitalini. Jipende, Ujali mwili wako. Tukifanya hivyo miili yetu itakuwa salama. 

Nafsi ni roho yenye kuleta imani ndani yetu. Sisi huamini vitu mbali mbali kwa msaada wa nafsi. Lakini yote heri kama tutaamini vitu vyenye kujenga na sio kubomoa. Nafsi pia hutofautiana ya mtu na mwingine ndio maana tukawa tofauti japo chimbuko letu kiuumbaji ni moja. 

Nafsi nayo huhitaji utulivu ili kuupa mwili na akili nguvu za kuishi kwa afya. Pata muda wa kutulia ukiongea na WEWE kujua nini waweza fanya LAKINI, mshirikishe MUUMBA wako kwa yote kupata amani uitakayo moyoni na kwa wakuzungukao.

Hivyo basi, jipe likizo au omba likizo. Tembelea sehemu mbali mbali za starehe au vivutio kutuliza mwili, akili na roho pia. Ongea vizuri na watu, cheka, tabasamu hata kama umeumizwa. Inasaidia sana. 

Afya ya vitu vyote vitatu ni muhimu katika kukuweka mwenye nguvu na furaha.
 Jali afya yako!



Friday, July 8, 2016

KUWA MTU MZURI LAKINI USIPOTEZE MUDA KUTHIBITISHA




Tumeumbwa tupendane lakini haimaanishi umpende kila mmoja sawa sawa. Tunapaswa kusaidiana na kuheshimiana lakini inaposhindikana unaacha. Usiumize kichwa kumfurahisha asiyetaka au asiyestahili. Kakupotezea muache, usimlete karibu kilazima.

Asipokuona mzuri machoni mwake muache sababu wapo wengine maelfu zaidi wanaokuona uko sawa. Hajaona thamani yako muache sababu wapo wengi zaidi wanaotambua uwepo wako na hasa umuhimu wako. 

Timiza wajibu wako kwa kila mmoja katika jamii yako kulingana na nafasi yako kwao. Jali, heshimu, penda, sahihisha, funisha, ongoza, furahisha, onya, lakini kama haionekani kumsaidia unayemfanyia badilisha njia, mtazamo, suluhisho, matendo. Usilazimishe wala kung'ang'ania, utajiumiza.

Yamkini mia wakakusema vibaya, usiumie sababu yupo japo mmoja anayetambua uzuri wako kwa wema wako; na hilo ni kuu mno. Kuwa hivyo ulivyo na uache mengineyo yapite njia yake... 

Monday, July 4, 2016

MAZOEZI SI HAKIKA YA AFYA NJEMA



Mazoezi ni muhimu kwa kukuweka mwenye nguvu muda wote lakini maisha unavyoyaishi pia yanachangia katika kukufanya mwenye furaha, mchangamfu na mwenye afya njema.

Dr. Denis Nturibi anasema kuna vitu vitatu ambavyo binadamu wote tunapaswa kuvifuata ili kuwa na afya njema. Mazoezi ni sahihi kuyafanya lakini muundo wa maisha (lifestyle) yetu unamchango mkubwa pia.

1. Kula sahihi.
Tunapaswa kupata lishe bora kwa maana kwamba tuachane na vyakula ambavyo vinanenepesha hasa vyenye mafuta mengi na sukari nyingi. Tusile sana yaani tule kwa kiwango na kwa muda tu. Kuna watu wanakula kwa siku hata zaidi ya mara nne. Kila unachoona unataka uonje. Basi tujitahidi kujiwekea mipaka yaani nini kiliwe na kwa muda na kiwango gani, Bila kusahau maji ya kunywa (angalau lita moja kwa siku).

2. Pumzika na lala.
Tunafanya kazi kupata hela, sawa kabisa. Hata Mungu anatuambia tufanye kazi na ametuweka duniani hasa kufanya kazi bila hivyo hatupati kula. Lakini kila kitu kiwe kwa kiasi. Pata muda wa kutosha wa kupumzika. Kazi nyingi zinatufanya tutumie akili sana katika kufikiria, kusuluhisha na kudadavua mambo kitu ambacho huchosha sana akili na mwili pia. 
Lala masaa yanayotakiwa (8-10). Usitumie muda mwingi kuangalia luninga ukakesha asubuhi unaelekea darasani au ofisini. Usisome masaa tisa ukalala kwa saa moja au kuvusha kabisa halafu uingie kufanya mtihani. Pumzika  na lala ili akili pia ipumzike na mwili kwa ujumla.

3. Shughuli za kimwili.
Mazoezi ya viungo ni muhimu katika kukufanya mwepesi. Kimbia taratibu (jogging) au tembea kwa mwendo wa haraka kwa umbali kidogo kila siku au walau mara mbili kwa wiki. Hii itakusaidia kukupa pumzi nzuri. Kwa wale waimbaji, sauti yako itapunguza kuhema hema.


Kwahiyo, Dr. Dennis anaeleza vizuri kuwa, mazoezi pekee si afya, lishe na kupumzika pamoja na kulala vinasaidia kwa afya bora.

Unaweza kuwa na mwili mdogo na wenye nguvu sababu ya mazoezi lakini kama unakunywa pombe sana au unavuta sigara utakuwa na nguvu bila afya njema.

Jitengenezee mazingira mzuri ya kuwa na afya muda wote kwani afya njema ndio kila kitu.




Unaweza kushindwa kudhibiti tabia hasi za mtu. Lakini unaweza kudhibiti muda gani unashiriki ndani yake.


Toka upate ufahamu wa kunyambua mambo, leo hii jiulize umeachana na wangapi? Jana ulikuwa na rafiki huyu lakini leo uko na mwingine. Uwezo wa kuwa na mwingine ndio unaoonesha ujasiri wako kwani hukutaka kuvumilia kuwa na mtu ambaye hana nia nzuri na wewe ama faida katika maisha yako.

Binadamu tunatofautiana sana. Haiwezekani ukakutana na mtu ambaye utafanana naye kila kitu lakini unaweza kuwa na mtu au watu ambao mtakuwa na tabia japo chache zinazorandana. Unapokutana na mtu au watu msiowezana hasa kitabia muache mara moja asijekukuumiza kichwa. Jinsi unavyoendelea kubaki naye ndivyo utakavyokwazika ama kuteseka. 

Haijalishi anakupa pesa kiasi gani, mali za thamani, utambulisho kwa watu wazito/vigogo. Kama hakupi furaha, hakuonyeshi upendo, hana muda ma wewe basi fanya hima uachane naye. Tunaishi mara moja, usivumilie ukidhani utabahatika kuwa na "part two" kuishi...mkimbie. Fikiria mara mbili kisha fanya maamuzi sahihi na ya haraka. Unaweza...